Historia ya wakimbizi wa Poland waliokimbilia Tengeru

0
18

Wakati wa Vita ya Pili ya Dunia, Poland ilikuwa chini ya uvamizi, maelfu ya Wapoland walipata hifadhi katika maeneo tofauti ulimwenguni na wengine wakafanikiwa kufika Afrika.

Walitawanyika katika vijiji zaidi ya ishirini katika nchi sita katika Afrika ya Mashariki na Kusini mwa Afrika na moja ya maeneo hayo ilikuwa Tanganyika, sasa inayojulikana kama Tanzania.

Kundi moja la takribani watu 5,000 lilipata makazi huko Tengeru, Arusha likiwa na matumaini ya kuanza upya maisha yao. Lakini maisha yalikuwa magumu, pamoja na vifo vingi vilivyosababishwa na magonjwa ya kutisha kama malaria ambayo Wapoland hawakuwa wamezoea.

Wakimbizi waliishi kwa kwa amani na kuwa wenyeji wa eneo hilo, baada ya hapo baadhi waliendelea na safari yao, wakapata makazi Uingereza na Marekani, huku wengine takribani 1,000 wakiamua kubaki na kuiita Tengeru nyumbani kwao, wakawa sehemu ya jamii ya Tengeru.

Hata hivyo, katika uwanja mdogo uliofichwa mbali na macho ya watu, kuna kaburi dogo lililozungushiwa ukuta ambapo wakimbizi 149 wamezikwa.

Leo, makaburi haya yamekuwa kama alama ya urafiki kati ya Tanzania na Poland na watu kutoka pande zote huenda kutoa heshima zao kwa wakimbizi hao waliofariki, wakiwa na ufahamu kwamba historia hii haiwezi kusahaulika.

Mtanzania, Simon Joseph mzee wa kijiji amechukua jukumu la kuyatunza makaburi hayo kwa kujitolea na kuhakikisha kwamba historia hiyo haipotei. Kila mwaka, watu kutoka maeneo mbalimbali hufika kusikiliza hadithi hizi na kutoa heshima zao kwa waliotangulia.

Joseph alirithi eneo hilo kutoka kwa baba yake ambaye aliishi na kufanya kazi na jamii ndogo ya Kipolishi kwa miaka mingi.