Jeshi la Polisi lawafariji wafungwa Gereza la Segerea

0
24

Askari wa Jeshi la Polisi kutoka Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA) wamewafariji mahabusu na wafungwa katika Gereza la Segerea kwa kuongea nao na kuwapa vitu mbalimbali lengo likiwa ni kutambua kundi hilo muhimu katika taifa.

Mwenyekiti wa Mtandao wa Polisi Wanawake kutoka DPA, Anitha Semwano amesema wanatambua umuhimu wa kundi hilo katika jamii hivyo wao kama Jeshi la Polisi wametumia Siku ya Wanawake Duniani kuwapa elimu ya ukatili wa kijinsia na namna ya kutoa taarifa za ukatili katika jamii.

Aidha, amesema kundi hilo lipo gerezani hapo kwa mujibu wa sheria kwa kuwa walikinzana na sheria za nchi hivyo kupelekea kuwa katika mazingira hayo.

Naye Mratibu wa Magereza, SP Iyunge Saganda amesema mchango wa askari hao utakuwa msaada mkubwa kwa wafungwa hususani wafungwa wanawake na kutoa wito kwa taasisi nyingine kuiga mfano mzuri wa Jeshi la Polisi kwa kuyakumbuka makundi yenye uhitaji.