Kauli ya kwanza ya Polepole baada ya kufungiwa na TCRA

0
16

Mbunge Humphrey Polepole amesema kazi ya kusema ukweli ina safari kidogo lakini hatokatishwa tamaa na uamuzi wa Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kukifungia kipindi cha Shule ya Uongozi.

Polepole amesema hayo muda mfupi baada ya hukumu hiyo ya kufungia kwa muda kipindi hicho kilichokuwa kikiruka kupitia Humphrey Polepole Online Television.

TCRA yakifungia kipindi cha Shule ya Uongozi cha Humphrey Polepole

“Kazi ya kusema kweli ina safari kidogo… Kwangu mimi hii mitihani midogo. Nitakaa na wasaidizi wangu, tutatafakari hukumu hii iliyotolewa leo na nitawajulisha hatua ambayo itafuata,” amesema.

Ameongeza kwamba yeye kama mwanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) anasimamia ahadi ya kusema ukweli siku zote bila kuweka chembe ya fitna kwa sababu anaamini anachofanya ni kwa maslahi ya Taifa.

Amesema pia anasimamia ahadi inayosema “nitafanya jitahada kujielimisha na kutumia elimu kwa faida ya wote.”

“Mimi binafsi sitokata tamaa maadamu ninachokifanya kinalinda maslahi mapana ya nchi yetu Tanzania na watu wake, mamlaka ya nchi na chama chetu cha mapinduzi,” amehitimisha mbunge huyo.

 

Send this to a friend