Maalim Seif afungiwa kufanya kampeni kwa siku tano

0
14

Kamati ya Maadili ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imemfungia mgombea Urais wa Zanzibar kupitia ACT-Wazalendo, Seif Sharif Hamad kutofanya kampeni kwa siku tano.

Adhabu aliyopewa mgombea huyo anayeisaka nafasi hiyo kwa mara ya sita inaanza Oktoba 16 hadi Oktoba 20, 2020.

Kamati hiyo imefikia uamuzi huo kutokana na malalamiko yaliyowasilishwa na chama cha Demokrasia Makini kuwa mgombea huyo amekuwa akiwashawishi watu wapige kura Oktoba 27, 2020 kinyume na utaratibu, kwani siku ya watu wote kupiga kura ni Oktoba 28.

Zanzibar inatarajiwa kupiga kura ya mapema Oktoba 27, 2020 ambapo makundi maalum tu ndiyo yatakayohusika. Hata hivyo ACT-Wazalendo imekuwa ikitilia shaka usalama wa kura hizo hasa zitakapowekwa usiku wa kuamkia siku ya uchaguzi.

Maalim Seif anakuwa mwanasiasa wa pili kufungiwa kufanya kampeni baada ya mgombea Urais wa Tanzania kupitia CHADEMA, Tundu Lissu kufungiwa siku saba na Kamati ya Maadili Kitaifa.

Send this to a friend