Mambo matatu wakazi wa Dar wasiyotakiwa kufanya katika kipindi chote cha Mkutano wa SADC

0
16

Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es salaam limejipanga kuimarisha ulinzi wakati wa Mkutano wa 39 wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) utakaofanyika jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo ambao umeanza leo tarehe 05 August,2019 utaendelea hadi tarehe 18 August 2019 na utahudhuriwa na wakuu wa nchi 16 wanachama wa Jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini mwa afrika (SADC).

Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es salaam limejipanga kikamilifu kuhakikisha amani na utulivu vinatawala kipindi chote cha mkutano huo.

Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama tumejipanga kukabiliana na kikundi chochote au mtu yeyote atakaejaribu kufanya vitendo vya uhalifu au kuvuruga amani na utulivu katika kipindi chote cha mkutano.

Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam linawahakikishia usalama wageni wote waliokuja kwenye mkutano huu katika kipindi chote na kwamba wawe uhuru kutembea mahali popote pale ndani ya Jiji la Dar es Salaam kwani hali ni shwari kabisa.

Aidha katika kipindi hiki cha mkutano wa SADC Jeshi la polisi kanda maalum Dar es Salaam linapiga marufuku mambo yafuatayo;

✓ Marufuku pikipiki (Bodaboda )zote kuingia katikati ya Jiji kuanzia tarehe 06 August hadi 18 August, 2019.Kutokana na sababu ya baadhi ya bodaboda kujihusisha na vitendo vya uhalifu ,Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limepiga marufuku bodaboda kufika maeneo yote ya katikati ya Jiji.

✓ Marufuku kuweka taa za vimulimuli au za rangi rangi, taa zenye mwanga mkali (spot light) na kufunga ving’ora kwenye Magari ya kiraia au watu binafsi na pikipiki zote za kiraia, isipokuwa magari yanayotoa huduma za dharura tu na ya makampuni binafsi ya Ulinzi.

✓ Marufuku kuingilia misafara ya wageni, wananchi wanatakiwa kuwa wavumilivu kipindi hiki cha ugeni mkubwa wa kimataifa.

Pia wananchi wote wanatakiwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili kuimarisha ulinzi na usalama katika Jiji la Dar es salaam

Send this to a friend