Mashabiki Simba vs Yanga kurudishiwa tiketi

0
12

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa ameagiza mashabiki 43,947 waliokata tiketi kwenye mchezo wa Simba SC na Yanga SC ambao uliahirishwa Mei 8, 2021 kurejeshewa tiketi zao kwenye mfumo wa kadi za kuingilia uwanjani.

Bashungwa ametia agizo hilo na kuelekaza kuwa mashabiki hao watatumia tiketi hizo hizo kuingia uwanjani na kukaa eneo lile lile alilokaa awali siku na tarehe itakayopangwa kurudiwa mechi hiyo.

Aidha, amesema mfumo huo wa N-Card unaosimamiwa na Kituo cha Taifa cha Data uwaruhusu mashabiki wengine ambao awali hawakukata tiketi waweze kukata tiketi za mchezo huo endapo watataka na kukidhi idadi inayoruhusiwa kulingana na uwezo wa uwanja.

Maamuzi hayo yametokana na kikao cha pamoja kilichofanyika mkoani Dar es Salaam kati ya wizara hiyo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Bodi ya Ligi, Baraza la Michezo Tanzania na klabu za Simba na Yanga.

Waziri Bashungwa amewaomba radhi mashabiki wa soka nchi kutokana na kusogezwa mbele na baadaye kuahirishwa kwa mchezo kati ya Simba SC na Yanga SC.

Aidha, amezitaka TFF na Bodi ya Ligi zikae haraka iwezekanavyo il kutoa tarehe mpya ya kuchezwa kwa mchezo huo.

Send this to a friend