Mashine 7 za kuzalisha umeme Ubungo hazifanyi kazi

0
15

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga ametoa saa mbili kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha linatengeneza mitambo ya kuzalishia umeme ya kituo cha kuzalisha umeme cha Ubungo 1 ambayo ilipata hitilafu usiku wa kuamkia leo Septemba 29.

Ameyasema hayo wakati alipotembelea vituo vya kuzalisha umeme vya Ubungo 1 na Ubungo 2 ambapo amewataka TANESCO kuwa na mpango madhubuti wa kufanya marekebisho kwa muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu, ili kuwawezesha kufanya matengenezo kwa haraka na kurejesha upatikanaji wa umeme wa uhakika.

“Na leo kituo cha ubungo 1 kimezimika umeme kuanzia usiku mpaka sasa hivi na mitambo ile sita ambayo inatakiwa kuzalisha umeme kwa sasa hivi haizalishi lakini wataalamu wapo saiti wanahakikisha inawaka, na nimewaelekeza TANESCO kuhakikisha ndani ya saa mbili kituo kile kinarudi katika uzalishaji, na kama hakitorudi kwenye uzalishaji watafute njia mbadala ya kuhakikisha ndani ya saa sita zijazo kituo hicho kiwe kimerudi kwenye uzalishaji ili hali ya upatikanaji umeme iimarike” amesema.

Aidha, ameeleza kuwa katika kituo cha kuzalisha umeme cha Ubungo 2 kuna mashine mbili zinazofanya kazi kati ya tatu ambazo zina uwezo wa kuzalisha MW 43 kila moja, vile vile katika kituo cha Ubungo 1 kuna mashine 12 za kuzalisha umeme na kati ya hizo mashine sita pekee ndizo zinaendelea kufanya kazi na mashine sita zikiwa  na hitilafu.