
Mfuko wa Mikopo (Self Microfinance Fund) umesema katika kipindi cha miaka mitano ijayo (2026 hadi 2030) mfuko umejipanga kutoa mikopo ya shilingi bilioni 300 pamoja na kuongeza idadi ya wanufaika wa mikopo hiyo hadi kufikia watu 200,000.
Ameyasema hayo Afisa Mtendaji Mkuu wa mfuko huo, Santieli Yona wakati wa mkutano na waandishi wa Habari na wahariri chini ya uratibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina jijini Dar es Salaam.
“Mwaka 2021 hadi Juni 2025, mfuko umetoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 196.9 ambapo katika utoaji wa mikopo hiyo, mfuko umeweza kuhakikisha kiwango cha mikopo chechefu hakizidi asilimia 10,” amesema.
Ameongeza kuwa huduma za mikopo zinawafikia Watanzania katika maeneo yote, ambapo katika kipindi cha mwaka 2021 hadi Juni 2025 mfuko umeweza kuwafikia wanufaika wapatao 183,381 na kati ya hao, 97.170 sawa na asilimia 53 ni wanawake, na 86,211 ni wanaume ambao ni sawa na asilimia 47.
Mbali na hayo Bi. Yona amesema mfuko huo umepata mafanikio mbalimbali ikiwemo kutengeneza ajira takribani 183,000 pamoja na kutoa mikopo wa ajili ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni ajenda ya Rais Samia Suluhu Hassan
Haya hivyo, ametoa rai kwa wananchi mbalimbali nchini kufanya tathimini ya kina kabla ya kuchukua mkopo, kukopa kwa malengo pamoja na kurudisha kwa wakati ili kujiwezesha kujikwamua kiuchumi.







