Mjamzito afariki baada ya kuhudumiwa na daktari anayedaiwa kuwa mlevi

0
12

Baraza la Madaktari Tanganyika limesema linafanya uchunguzi wa kifo cha mama mjamzito, Dainess Masawe ambaye anadaiwa kuhudumiwa na daktari msaidizi aliyekuwa katika hali ya ulevi katika kituo cha afya cha Ngarenairobi wilayani Siha Kilimanjaro.

Katika taarifa iliyotolewa kwa umma na baraza hilo Septemba 29, 2023 imebainisha kuwa daktari huyo msaidizi wa kituo amedaiwa pia kuchelewa kutoa huduma kwa mama huyo na kupelekea kifo chake, hivyo baraza limewakumbusha wataalamu wa afya kutoa huduma stahiki na kwa wakati kwa wagonjwa.

“Baraza linaendelea kuwakumbusha wanataaluma ya udaktari, udaktari wa meno na afya shirikishi kutoa huduma stahiki na kwa wakati kwa wagonjwa kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni za kitaaluma, pamoja na kutumia taaluma zao kutibu watu,” imeeleza taarifa hiyo.

Waziri Ummy asema Serikali haijafuta Toto Afya Kadi

Aidha, baraza limetoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu kwa kuondokewa na mpendwa wao pamoja na kuwasihi wananchi wa wilayani Siha kuwa watulivu na wavumilivu katika kipindi hiki ambacho kwa kushirikiana na vyombo vingine linafanya uchunguzi wa kitaalamu kubaini kilichopelekea kifo cha marehemu.