Mtoto amuua mama wa kambo kisa mali za baba yake

0
17

Watu watatu akiwemo mama mjamzito wameuawa katika kitongoji cha Kilimahewa, kata ya Ludete katika mji mdogo wa Katoro mkoani Geita ambapo wawili wanasadikiwa kuwa ni majambazi waliovamia familia ya Msafiri Renatusi usiku wa kuamkia leo.

Tukio hilo limetokea majira ya saa mbili usiku ambapo mama mjamzito aliyetambulika kwa jina la Elinata Elias (27) ameuawa kwa kuchinjwa shingo na kitu chenye ncha kali huku baba wa familia hiyo, Msafiri Renatus akijeruhiwa vibaya.

Mashuhuda wa tukio hilo wamesema majambazi hao, akiwemo mtoto wa kiume wa Msafiri Renatus aliyetambulika kwa jina la Jackson Msafiri (25) akiwa na rafiki  ambaye jina lake halijafahamika walifika katika familia hiyo na kutekeleza mauaji ya mama huyo.

Taharuki Dodoma na Singida baada ya kukumbwa na tetemeko mara tatu

Baada ya kutekeleza mauji hayo majambazi hao waliuawa na wananchi wenye hasira kali waliokuwa na silaha za jadi ambao walikuwa wamezingira nyumba ya Msafiri.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha  Kilimahewa, Michael Chuma  pamoja na msemaji wa familia, Mihayo Renatus wamesema chanzo cha kijana huyo kutekeleza mauaji  hayo pamoja na rafiki yake ni tamaa za mali ya baba yake ambaye aliachana na mama yake kisha kuoa mwanamke mwingine.

Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Katoro, Dkt. Zakayo Sungura amethibitisha kupokea miili ya watu hao watatu pamoja na baba wa familia hiyo ambaye alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita kwa ajili ya matibabu zaidi.