Mtoto wa miaka 14 ashikiliwa kwa tuhuma za kubaka na kulawiti watoto

0
28

Jeshi la Polisi linamshikilia mtoto wa miaka 14 (jina linahifadhiwa) mkazi wa Kijiji cha Mnete, kilichopo Kitongoji cha Chiano, Kata ya Nalingu, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara kwa tuhuma za kuwabaka watoto wawili wakiwemo binti wa miaka 7 na kumlawiti mtoto wa kiume wa miaka mitano.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Nicodemus Katembo amesema tukio hilo limetokea Oktoba Mosi na Oktoba 15, mwaka huu kwa nyakati tofauti ambapo mtuhumiwa anatuhumiwa kumbaka mtoto wa kike na kumlawiti mtoto wa kiume wote wa familia moja, wakazi wa Nalingu na kuwasababishia maumivu katika sehemu zao za siri.

“Waathirika wote wawili wamefanyiwa uchunguzi wa kitabibu na wanaendelea vizuri, mbinu iliyotumika ni kuwavizia nyakati za usiku wakiwa wamelala kisha kuwaingilia mmoja baada ya mwingine na kiini cha tukio ni tamaa za kimwili,” ameeleza.

Akizungumza mama mzazi wa watoto hao ameeleza kuwa Alhamisi Oktoba 19, 2023 akiwa kazini alipigiwa simu kuwa watoto wake wamefanyiwa ukatili huo na mdogo wake wa kiume, na kwamba mtuhumiwa alipohojiwa alieleza kuwa huwafanyia vitendo hivyo kila mara pindi dada yake [mama wa watoto hao] anapotoka nyumbani.