Mwanamke akiri kumnywesha sumu mtoto mchanga wa jirani yake

0
13

Jeshi la Polisi mkoani Tabora linamshikilia mwanamke aliyetajwa kwa jina la Wande Shija, mkazi wa Mtaa wa Mbagala B, Kitongoji cha Magharibi kwa tuhuma za kumnywesha sumu mtoto wa siku moja wa jirani yake.

Mama mzazi wa mtoto huyo, Kashinje Julius amesema mwanaye alinyweshwa sumu Machi 19, mwaka huu wakati yeye akiogeshwa na dada yake mara baada ya kutoka kujifungua katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga.

“Wakati tukiendelea kuoga ghafla tulisikia kilio kikali cha mtoto na kuamua kuvaa nguo haraka. Tulipofika chumbani mtoto aliendelea kulia kwa mfululizo, na dada alipombeba alisikia harufu kali bila kujua ni nini na inatoka wapi. Mimi na dada tulianza kumnusa mwilini, na ndipo tulibaini kuwa mdomoni kuna harufu kali ambayo hatukuweza kufahamu kwa haraka ni nini,” ameeleza.

Ameongeza kuwa wakati wa tukio hilo kulikuwa na watu wanne; akiwemo yeye, dada yake, mdogo wake pamoja na jirani yao ambaye ndiye mtuhumiwa, na baada ya kwenda hospitali madaktari walijaribu kuokoa maisha ya kichanga hicho lakini kwa bahati mbaya alifariki dunia.

Hata hivyo, mama huyo ameeleza kuwa manesi waliwahoji kwa pamoja kwa takribani saa mbili na Wande alikiri kumnywesha sumu mtoto huyo.

Kwa upande wa Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Igunga, Melchades Magongo amekiri kumpokea kichanga hicho akiwa anatapika na kushindwa kupumua huku mdomoni akiwa na harufu inayodhaniawa kuwa ni sumu, na kufikia Machi 29, mwaka huu aliaga dunia.

Send this to a friend