Mwanaume adaiwa kumkata mikono mtalaka wake aliyekwenda kwake kuchukua mali

0
16

Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Mtwara, Nicodemus Katembo amethibitisha kufikishwa mahakamani Shaibu Ally Mtepa (61) kwa tuhuma za kujaribu kumuua mtalaka wake, Fadina Mussa (47) kwa kumkata mapanga mikono yote miwili na kumjeruhi shingoni na kichwani.

Akizungumza mkoani humo, Kaimu Kamanda huyo amesema kuwa tukio hilo lilitokea katika Kijiji cha Maropokelo, Wilaya ya Tandahimba mkoani Mtwara Desemba 3, 2021, ambapo Fadina alikwenda nyumbani kwa mtuhumiwa kwa lengo la kuchukua mgawanyo wa mali.

“Mama huyo alikwenda kwa mumewe huyo wa zamani akiwa na Afisa Mtendaji wa kata kwa lengo la kuchukua sehemu ya mgao wa mali baada ya kuachana, ndipo mwanaume akatoka na panga na kuanza kumshambulia,” amesema Katembo.

Hata hivyo Katembo ametoa rai na kuwataka wanajamii wote kuheshimu maamuzi yanayotolewa na vyombo vinavyotoa haki, na kuepuka kujichukulia sheria mikononi.

Send this to a friend