Padri kizimbani kwa tuhuma za wizi milioni 20

0
18

Padri Baltazar Sulle (63) ambaye ni Paroko wa Parokia ya Haydom, Kanisa Katoliki Jimbo la Mbulu Mkoa wa Manyara amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara kwa madai ya wizi wa TZS milioni 20 za kaka yake.

Akisomewa mashitaka hayo na Wakili wa Serikali mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Mwandamizi, Mariam Lusewa amedai Paroko huyo anadaiwa kuiba fedha hizo kwenye akaunti ya kaka yake aitwaye Dionis Margwe huku akishirikiana na wafanyakazi wawili wa Benki ya NMB.

Mshitakiwa anadaiwa kuchukua fedha hizo ambazo zilitokana na mirathi ya shemeji yake na kaka yake ambaye alishafariki dunia huku akidaiwa kutenda kosa hilo Machi 3, 2021 kwa kushirikiana na wafanyakazi hao waliotajwa kuwa ni Cynthia Nyamtiga (27) na Winfrida Rwakilomba (30).

Serikali yaeleza chanzo cha kifo cha mwandishi wa TBC aliyefia Ml. Kilimanjaro

Katika shtaka la pili linalomkabili Paroko huyo ni kughushi nyaraka kinyume na kifungu cha 333 na kifungu cha 355 (a) na kifungu cha 335 (d) (i).

Washtakiwa wote watatu wako nje kwa dhamana baada ya kutimiza masharti kwa kulipa bondi ya TZS milioni saba kwa kila mdhamini na kesi hiyo kuahirishwa hadi Desemba 21, mwaka huu.

Chanzo: Nipashe