Polisi wamwamuru mwandishi wa Mwananchi kubembeleza mawe kama mtoto

0
13

Gazeti la Mwananchi limeripoti kuwa mwandishi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL) Zanzibar, Jesse Mikofu jana alishambuliwa na askari wa vikosi vya SMZ wakati akitekeleza majukumu yake ya kazi.

Mikofu alikumbwa na kadhia hiyo baada ya kuwapiga picha askari hao wakati wakitekeleza jukumu lao la kuwahamisha wamachinga waliopanga bidhaa zao barabarani katika eneo la darajani.

Amesema kuwa aliamuriwa kujigaragaza kwenye maji machafu, kupakata mawe makubwa na ayabembeleze kama mtoto, huku vifaa vyake vya kazi ikiwemo simu vikiharibiwa.

“… niliambiwa nikae chini ninyooshe miguu, nipakate mawe makubwa wakiniambia niyabembeleze kama mtoto,” amesema.

Mbali na hilo amesema aliamriwa kubadili nywila ya simu yake, alipokataa, askari mmoja aliibadili, ndipo Mikofu alipoamriwa kuipiga simu yake kwenye jiwe hadi ikaharibika.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Awadh Juma Haji amesema hana taarifa za tukio hilo na kuahidi kutoa ushirikiano zitakapomfikia.