
Mkazi wa Kitongoji cha Mgomwa, Kata ya Matumbulu jijini Dodoma, Frank Sanga (32), amefariki dunia baada ya kudaiwa kupigwa risasi na askari polisi waliokuwa kwenye doria, alipokuwa akijaribu kumsaidia ndugu yake aliyekamatwa kwa makosa ya usalama barabarani.
Tukio hilo limetokea Julai 19, 2025, majira ya saa 7:30 mchana katika maeneo ya Matumbulu, ambapo Frank alijeruhiwa kwa risasi kwenye paja na kwenye kisigino cha mguu wa kushoto. Alikimbizwa hospitalini kwa matibabu, lakini baadaye alifariki dunia akiwa bado anaendelea kupatiwa matibabu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gallus Hyera, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa askari wawili wanaoshukiwa kuhusika wamekamatwa na wanashikiliwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi, japokuwa majina yao hayajawekwa wazi.
Kwa mujibu wa Kamanda Hyera, siku ya tukio askari walimkamata dereva wa pikipiki (ambaye jina lake limehifadhiwa kwa sababu za kiuchunguzi) kwa makosa ya kuendesha pikipiki bila leseni, kutovaa kofia ngumu na kuendesha chombo kibovu.
Baada ya kukamatwa, dereva huyo alipiga simu kwa ndugu zake ambao walifika eneo la tukio kwa pikipiki tano, kila moja ikiwa imebeba watu zaidi ya wawili. Walidaiwa kuanza kulazimisha kuichukua pikipiki hiyo kwa nguvu na kutaka ndugu yao aachiwe huru bila kuchukuliwa kituoni.
Kamanda amesema askari walilazimika kujihami kwa kufyatua risasi, ambapo Frank alipigwa risasi na kujeruhiwa vibaya.
Chanzo: Mwananchi








