Polisi watilia shaka kujinyonga kwa mwenye ulemavu wa mikono na miguu

0
13

Jeshi la Polisi mkoani Mtwara linasema linatilia shaka tukio la kujinyonga kwa binti Samia Ahmed Mohamed (20) mkazi wa Kijiji cha Sinde Kata ya Msangamkuu Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara kutokana na hali yake ya ulemavu wa mikono na miguu aliyonayo.

Akizungumza, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi, Mtaki Kurwijila amesema kuwa tarehe 11 Septemba mwaka huu, majira ya saa saba mchana, binti huyo aligundulika amefariki dunia pembeni mwa jiko la nyumbani kwao, huku mwili wake ukiwa umelala kifudifudi ukivuja damu mdomoni na puani.

Mkuu wa Wilaya shitakiwa kwa kutusi na kuwaweka mahabusu watumishi

“Baada ya kuukagua mwili, ulikuwa umefungwa na kamba ya manira shingoni, kama mtu aliyejinyonga. Upelelezi wa awali, Jeshi la Polisi limebaini kutokana na ulemavu wa mikono na miguu aliokuwa nao Samia, uwezekano wa yeye kujinyonga ni mdogo,” ameeleza Kamanda.

Ameongeza kuwa binti huyo hakuwa na uwezo wa kutembea, hali inayozidi kuleta shaka kama kweli amejinyonga mwenyewe, hivyo jeshi la polisi linamshikilia babu yake kwa ajili ya mahojiano zaidi, huku mwili wa marehemu ukihifadhiwa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara kwa ajili ya uchunguzi.