Precision Air yarejesha safari za Dar – Tabora

0
13

Shirika la ndege la kitanzania, Precision Air limerejesha safari zake za Dar es Salaam – Tabora rasmi kuanzia leo Januari 31, 2022 baada ya kuzisitisha kwa takribani mwaka mzima.

Precision Air itakua ikifanya safari zake mara tatu kwa wiki, kila Jumatatu, Jumatano na Ijumaa ndege  ikiondoka Dar es Salaam saa 12 asubuhi na ikitoka Tabora saa 3 Asubuhi.

Akizungumza kuhusu kurudi tena kwa safari hizo, Meneja wa Masoko na Mawasiliano, Hillary Mremi amesama safari hizo zimerejeshwa kimkakati baada kusitishwa kwa mda na kwamba kurejeshwa kwa safari hizo kumekuja kwa wakati muafaka kukidhi mahitaji  ya usafiri wa anga kwa wakazi wa Tabora.

“Tumepokea maombi mengi kutoka kwa wakazi na wafanyabiashara wa Tabora, wakihitaji huduma za usafiri wa anga za uhakika na nafuu na kwa kuwa sisi ni shirika la kitanzania ambalo tumejidhatiti kuwahudumia Watanzania, tunawaahidi huduma bora na za uhakika,” ameongeza Mremi

Akifafanua Zaidi juu ya safari hizo, amesema safari za Tabora sasa zitakua zikipitia Dodoma, hivyo kufungua fursa nyingine kwa wakazi wa Dodoma, Tabora na maeneo ya jirani kupata huduma za usafiri wa anga kati ya Dodoma na Tabora.