Punguzo la tozo za miamala kuanza Septemba 7

0
11

Serikali imesema kuwa imetoa muda wa siku saba kuanzia Septemba 1 hadi 7 mwaka huu kwa kampuni za simu ziwe zimerekebisha mifumo yao ya makato ili punguzo la makato la asilimia 40 lililotangazwa na serikali lianze kutekelezwa.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa leo wakati akitoa taarifa za mwenendo wa serikali kwa kipindi cha wiki moja iliyopita, jijini Dodoma.

Msigwa amesema kuwa serikali ilisikia kilio cha wananchi kuhusu ukali wa tozo hizo na ikapunguza kwa 40% (30% serikali na 10% mitandao ya simu). Ametumia jukwaa hilo kuwasisitiza wananchi kuwa fedha zote zinazokusanywa katika tozo hizo zinatumika kwenye miradi ya kijamii (afya, elimu, maji, barabara).

“Fedha hizi pia zimepelekwa maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kujenga na kumaliza maboma ya vyumba vya madarasa 560 kwa ajili ya wanafunzi wetu ambao wataanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza mwakani,” amefafanua Msigwa.

Kuhusu tija ya tozo hizo amesema zimewekwa ili kuharakisha utatuzi wa changamoto za wananchi kwani serikali ikiendelea kwa kasi iliyokuwepo ingeweza kutumia muda mrefu zaidi kuikamilisha.

Send this to a friend