Rais Dk Magufuli aitisha mkutano na wafanyabiashara

0
14

Rais Dk John Pombe Magufuli ameitisha mkutano na wafanyabiashara ambao unatarajiwa kufanyika Ijumaa Juni 7, 2019, ambapo Rais atakutana na kufanya mazungumzo na wafanyabiashara mbalimbali.

Katika mkutano huo unaotarajiwa kufanyika katika Ukumbi wa Mikutao wa Kikwete, Ofisi ya Rais, Ikulu unatarajiwa kuhudhuriwa na takribani wafanyabiashara 685, ambao ni sawa na wafanyabiashara watano kutoka kila wilaya ya Tanzania Bara.

Katika barua ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambayo SwahiliTimes imeiona ikielekezwa kwa wakuu wa mikoa yote ya Tanzania Bara, walitakiwa kuwasilisha majina ya wafanyabiashara watano ambao watahudhuria mkutano huo kutoka kila wilaya, ambapo mwisho wa kuwasilisha majina hayo ilikuwa ni jana, Juni 2, saa 6:00 mchana.

Kwa mujibu wa barua hiyo, taarifa za wafanyabishara zitakazowasilishwa, zijumuishe pia majina ya wafanyabiashara hao, namba zao za simu, pamoja na aina ya biashara wanayofanya.

Aidha barua imeeleza kuwa, endapo katika wilaya kuna mfanyabiashara mkubwa ambaye pia ni mwanasiasa, wakuu hao wa mikoa wasisite kumjumuisha katika orodha.

Hata hivyo wafanyabiashara hao watakaotoka maeneo mbalimbali kwenda Dar es Salaam wametakiwa kujigharamia.

Send this to a friend