Rais Magufuli atunukiwa nishani ya lugha ya Kiswahili

0
14

Rais Dkt. Magufuli ametunukiwa Nishani ya Juu ya Shaaban Robert ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wake katika kuikuza na kuiendeleza lugha ya Kiswahili ndani na nje ya Tanzania.

Nishani hiyo imetolewa leo jijini Dodoma katika siku ya pili ya maadhimisho ya lugha ya Kiswahili na kupokelewa na Naibu Waziri Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Abdallah Ulega amepokea nishani hiyo kwa Niaba ya Rais Magufuli.

Dkt. Magufuli ametunukiwa nishani baada ya kupendekezwa na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA), Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA), taasisi, vyama na idara za lugha ya Kiswahili.

Baadhi ya sifa zilizochangia Dkt. Magufuli kutunukiwa tuzo hiyo ni pamoja na kuongeza matumizi ya Kiswahili serikalini, kushiriki kuifanya lugha hiyo kuwa moja ya lugha rasmi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika.

Sifa nyingine ni serikali anayoingoza kufanya marekebisho ya Sheria ya BAKITA ya mwaka 1967 na kupitisha kwa kanuni za baraza hilo. Pia, kushauri baadhi ya nchi za Afrika kutumia lugha hiyo na kueleza kuwa Tanzania inatoa walimu wa kufundisha lugha hiyo kwenye nchi hizo.

Mbali na hilo, vyombo mbalimbali vya habari ikiwa ni pamoja na Mwananchi, Habarileo, Clouds FM, TBC1, TBC Taifa, Wapo Radio zimetunukiwa tuzo kutokana na mchango wao katika kukuza Lugha ya Kiswahili.

Send this to a friend