Rais Samia ashinda tuzo Afrika kwa kuendeleza miundombinu ya usafiri

0
14

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameshinda tuzo ya Africa Road Builders–Babacar Ndiaye kwa mwaka 2022, tuzo ambayo hutolewa kwa kiongozi wa Afrika aliyeonesha jitihada kubwa zaidi katika kuendeleza miundombinu ya usafiri.

Kamati inayoandaa tuzo hiyo imempongeza Rais Samia kwa uongozi wake na jitahada alizozionesha katika kuendeleza miundombinu ya usafiri ikiwemo barabara na reli.

“Tunatuma salamu zetu za pongezi kwa Rais Samia Suluhu Hassan na watu wa Tanzania,” imeeleza kamati hiyo.

Miongoni mwa miradi ambayo kamati hiyo imeonesha kuitambua ni pamoja na mradi wa TZS bilioni 673 zilizotolewa na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) kwa ajili kuimarisha usafiri wa barabara, reli na anga, mkataba wa ununuzi wa treni za mizigo na kuanza ujenzi wa njia za mzunguko jijini Dodoma.

Tuzo hiyo inayodhaminiwa na AfDB ilianzishwa kwa heshima ya Babacar Ndiaye, Rais wa AfDB kutoka mwaka 1985 hadi 1995.

Tuzo ya mwaka 2022 itatolewa katika mkutano wa mwisho wa Africa Road Builders ambao unatafanyika sambamba na mkutano wa mwaka wa AfDB Mei 2022 jijini Accra, Ghana.

Send this to a friend