Rais Samia: Timu ya Olimpiki ya Tanzania ina viongozi wengi kuliko wachezaji

0
12



Rais Samia Suluhu Hassan ameitaka Kamati ya Olimpiki kujitathmini na kuja na mkakati utakaowezesha kuongeza idadi ya washiriki katika mashindano mbalimbali tofauti na ilivyo sasa ambapo timu husafiri na viongozi wengi zaidi ya wachezaji.

Ametoa maelekezo hayo wakati akipokea Kombe la Ubingwa wa Michuano ya Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati kwa Vijana wenye umri chini ya miaka 23 (CECAFA Challenge Cup 2021), katika hafla iliyofanyika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam leo.

Agizo hilo limekuja siku chache tangu kumalizia kwa mashindano ya Olimpiki 2020 nchini Japan ambapo Tanzania ilipeleka wachezaji watatu, ambapo kati yao Alphonce Simbu ndiye alifanya vizuri zaidi kwa kushika nafasi ya saba katika mbio ndefu (42km) kwa wanaume.

Rais pia ametaka kuangaliwa vyema kwa wanamichezo nchini ili pindi wanapostaafu au kuumia wawe na maisha bora tofauti na hali ilivyo sasa  ambapo wengi wao wamekuwa na maisha duni yasiyo akisi mchango wao kwa Taifa.


Ameitaka sekta binafsi kuwekeza zaidi kwenye michezo nchini kwasababu imekuwa ni biashara kubwa duniani na kuipongeza Kampuni ya Azam Media Limited kwa namna inavyojitahidi kuwekeza kwenye mchezo wa mpira wa miguu na ndondi (vitasa) nchini.

Send this to a friend