Rais Samia: Vijana msisubiri Serikali itengeneze ajira

0
14

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewataka vijana kuacha kusubiri Serikali kutengeneza ajira badala yake kutafuta fursa zilizopo na kuzichangamkia ili nchi ipate maendeleo endelevu.

Hayo yamebainishwa leo wakati aliposhiriki kilele cha matembezi maalum ya UVCCM ya kuadhimisha miaka 59 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

“Nataka kuwaambia, kazi ya Serikali si kutengeneza ajira, ni kuweka mazingira mazuri ili vijana myatumie kutengeneza ajira na hiyo kazi tunaifanya vya kutosha. Naomba mwende mkatengeneze ajira kwa mazingira yaliyokuwepo,” amesema.

Aidha, ameeleza kuwa vijana wa leo wanakimbilia kwenye kupata utajiri lakini baada ya muda utajiri wao unakwisha kutokana na kukosa namna bora ya upatikanaji wa fedha kupitia miradi midogo midogo itakayoleta mzunguko wa fedha.

Katika hotuba yake, Rais Samia amesema Serikali imetenga bajeti ya kutosha kwenye sekta ya uzalishaji ili vijana waweze kuzalisha kupitia miradi mbalimbali ikiwemo kilimo na kukabiliana na upungufu wa chakula unaoweza kuikumba nchi kwa hapo baadaye.

Send this to a friend