Rais: Uhuru wa mahakama uende sambamba na uwajibikaji

0
38

Rais Samia Suluhu Hassan amesema hakuna taifa linaloweza kufikia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wake bila kuwepo kwa usimamizi mzuri wa haki unaosimamiwa na Mahakama huru, yenye uwezo na uadilifu.

Ametoa kauli hiyo leo Jumanne Januari 13, 2026 jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA), unaoongozwa na kauli mbiu “Jukumu la Mahakama Huru Katika Utoaji Haki.”

“Serikali itaendelea kuulinda na kuheshimu uhuru wa Mahakama, lakini uhuru huo hauna budi kuenda sambamba na uwajibikaji na maadili ya kazi,” amesema.

Akizungumzia suala la mishahara, Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza kuwa kadri uchumi wa nchi utakavyokua, ndivyo mishahara na stahiki za majaji na mahakimu itakavyoongezeka.

“Si kwamba hatutaki kuwafanya watu wote wawe na mishahara itakayowawezesha kuishi vizuri, lakini tuna limitations. Lakini nataka nisema tumejitahidi sana kwa kichache tunachokipata tunaongeza mishahara,” ameeleza.

Mbali na hayo, amesema imani ya Watanzania kwa mahakama imeongezeka hivyo ni tafsiri kwamba mahakama zinafanya kazi inayoridhisha.

Send this to a friend