Ripoti: Marekani yathibitisha kundi hatari la Mexico lilikuwa na maabara ya dawa za kulevya Kenya

0
4

Serikali ya Marekani imethibitisha kuwa kundi hatari la uhalifu kutoka nchini Mexico, Jalisco New Generation Cartel (CJNG), lilikuwa likiendesha maabara kubwa ya kutengeneza dawa za kulevya aina ya methamphetamine nchini Kenya.

Hii ni mara ya kwanza kwa kundi hilo kuthibitishwa kufanya shughuli zake Afrika Mashariki, jambo linaloashiria kujipanua kimataifa, kulingana na ripoti mpya.

Ripoti ya Kimataifa ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya iliyochapishwa Machi 2025. imesema maabara hiyo ilikuwa Namanga karibu na mpaka wa Kenya na Tanzania, na ilivunjwa mnamo Septemba 2024 baada ya operesheni ya pamoja ya vyombo vya usalama.

Ripoti imesema maabara hiyo ilikuwa imefichwa ndani ya jengo la mabati, jambo lililoruhusu cartel hiyo kufanya shughuli zake kwa siri, na kwamba ukaribu wake na mpaka wa Tanzania ulirahisisha upatikanaji wa njia za kusafirisha dawa hizo kimataifa.

Mamlaka bado zinachunguza ikiwa dawa hizo zilikuwa kwa matumizi ya ndani au zilipangwa kusafirishwa kwenda kwenye masoko nje ya nchi.

Kulingana na serikali ya Marekani, Kenya ina nafasi muhimu kijiografia kwani iko Pwani ya Afrika Mashariki, jambo linaloifanya kuwa njia rahisi ya kusafirisha dawa za kulevya kwenda Ulaya, Rasi ya Uarabuni, na maeneo mengine.

Kuanzishwa kwa CJNG nchini Kenya kunaonesha jinsi nchi hiyo inavyozidi kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji wa dawa za kulevya kimataifa.

Ingawa kumekuwa na ripoti za kupungua kwa kukamatwa kwa dawa za kulevya miaka ya hivi karibuni, maafisa wa Marekani wanaamini kuwa hii ni mbinu ya magenge ya ulanguzi ili kudhibiti bei na kuongeza faida.