Rushwa ya ngono ni kosa la uhujumu uchumi

0
26

Kwa mujibu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mtu atakayekamatwa kwa tuhuma za rushwa ya ngono, atafunguliwa shtaka la uhujumu uchumi.

Januari mwaka huu katika ufunguzi wa Wiki ua Sheria mkoani Kilimanjaro taasisi hiyo ilisema kosa la kuomba rushwa ya ngono sasa litafunguliwa shtaka kama kosa la uhujumu uchumi kutokana na matokeo ya rushwa hiyo katika utekelezaji wa majukumu na uzalishaji.

“Rushwa ya ngono inasababisha kupata wasomi ambao hawana sifa, pili kuajiriwa watu ambao hawana sifa na wenye sifa wanaachwa, na pia wale wanaoajiriwa uzalishaji wao na utendaji kazi ni mdogo na hivyo kusababisha uzalishaji mdogo na uchumi wa taifa kuwa mdogo,” alisema Mwanasheria wa TAKUKURU, Furahini Kibonga.

Akizungumzia hilo, Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika Mkoa wa Kilimanjaro, David Shillatu, alisema kama wadau wa sheria wanakubali kuwa rushwa ya ngono ipo kulingana na utafiti uliowahi kufanywa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hata hivyo alionyesha walakini kosa hilo kufanywa kuwa la kijinai.

‘‘Adhabu ya kushtakiwa kosa la rushwa ya ngono kama shauri la uhujumu uchumi ni adhabu kali sana…ni kosa la jinai ambalo halina hata dhamana,’’ alisema.