Serikali imesema inafanyia kazi suala la kikokotoo kwa waastaafu

0
13

Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango amesema Serikali imepokea hoja kuhusu kubadili kikokotoo kwa wastaafu, hivyo inafanya uchambuzi zaidi kuhusu hoja hiyo baada ya wafanyakazi kuonesha kutoridhishwa na uamuzi wa Serikali.

Akizungumza katika Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi yaliyofanyika kitaifa jijini Arusha, amesema ni muhimu kuzingatia kuwa uendeshaji na usimamizi wa mifuko ya hifadhi ya jamii ni suala la sayansi ya watakwimu-bima hivyo serikali inawategemea wataalamu hao waishauri kuhusu suala hilo la uhimilivu na uendelevu wa mifuko ya hifadhi ya jamii.

“Mheshimiwa Rais na Serikali yake tunaihakikishia wafanyakazi kwamba hakuna mtu angependa kuona watu waliotumikia nchi hii wakiathirika kwa kukosa kiinua mgongo stahiki au pensheni zao. Kutokana na hali hiyo, ndiyo maana Serikali iliposhauriwa na wataalam husika, Serikali ya Awamu ya Sita ilichukua uamuzi mkubwa wa kulipa deni la mifuko ya Hifadhi ya Jamii kiasi cha shilingi trilioni 2.147, hatua ambayo kwa kiasi kikubwa imeimarisha mifuko hiyo,” amesema.

Serikali yapiga marufuku uvutaji sigara maeneo ya wazi

Ameongeza kuwa “Serikali imepokea hoja kuhusu kubadilisha kikokotoo kwa ajili ya kuifanyia uchambuzi zaidi, maana kama ilivyosemwa kwenye risala, wafanyakazi hawaridhishwi na kanuni hizo. Hata hivyo, uamuzi wa kubadilisha Kikokotoo ni lazima utokane na tathmini ya kina ya kisayansi ya Watakwimu- bima.”

Aidha, katika suala la kuongezewa mishahara amewataka wafanyakazi wawe na matumaini kwamba Rais Samia Suluhu atasema jambo kuhusu ongezeko la mishahara kwa wafanyakazi ikiwa hali ya uchumi wa Tanzania itaendelea kuwa stahimilivu kwa kiasi cha kuridhisha.

Send this to a friend