Serikali kuchunguza vitabu vya shule vinavyohamasisha mapenzi ya jinsia moja

0
16

Serikali imesema inafuatilia suala la vitabu vya shule vinavyodaiwa kuwa na maudhui ya kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja kwa watoto na kutoa taarifa rasmi.

Hatua hiyo imekuja baada ya kusambaa kwa picha za vitabu hivyo kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii na kusababisha taharuki kubwa kwa wazazi hapa nchini.

Akizungumza na Mwananchi, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Omary Kipanga amesema hakuna taasisi yoyote yenye mamlaka ya kusambaza au kutumia vitabu bila kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania (TET).

“Tutafanya uchunguzi kuangalia ukweli wake halafu tutatoa kauli, lakini vitabu vyote vinavyotumika hapa nchini ni vile vilivyopata ithibati kutoka kwa Kamishna wa Elimu Tanzania na TET. TET ndiyo inaratibu vitabu vyote vya kujifunzia yaani kiada na ziada,” ameeleza.

Serikali yachunguza shule inayodaiwa kufundisha wanafunzi kulawiti

Aidha, Kipanga amesema kuwa kwa zile shule zinazotumia mitaala ya nje ya nchi zinapaswa kufahamu mambo yanayofundishwa kupitia vitabu hivyo kabla havijaanza kutumika mashuleni.

Baadhi ya picha hizo zinazosambaa zinaonyesha picha za kuchora za mwanaume na mwanamke wakiwa na mtoto, mwanaume na mwanaume wakiwa na mtoto pamoja na mwanamke na mwanamke wakiwana mtoto zikiashiria aina ya familia.