Serikali yapiga marufuku wanafunzi wa bweni kulala kitanda kimoja

0
14

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda amepiga marufuku kwa shule za bweni kuwalaza wanafunzi wawili katika kitanda kimoja na kuwaagiza walimu wakuu kutoa taarifa kwa wakurugenzi endapo vitanda ni pungufu.

Waziri Mkenda amesema hayo leo Desemba 15, 2022 Jijini Dodoma wakati wa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSA).

“Hakuna kutumia kitanda kimoja watoto wawili marufuku. Kama vitanda havitoshi tumwambie mkurugenzi, na mimi nitakuwa nalifuatilia, huyo mkurugenzi atakayekuwa anatumia hela sehemu nyingine halafu analaza watoto wa wazazi wenzake kitanda kimoja watoto wawili, huyo mkurugenzi anafaa kubaki ofisini?” amehoji.

Aidha, Waziri Mkenda amesema wakati wa kujadili masuala ya elimu ni vizuri kuzitambua na kuthamini juhudi zinazofanywa na walimu katika kuandaa wataalamu wa fani mbalimbali hapa nchini.

“Wajibu wa Serikali ni kuandaa mazingira mazuri ya utoaji elimu ili walimu waweze kufundisha katika mazingira mazuri na kuchochea ufaulu, amesema Waziri Mkenda.

Send this to a friend