Serikali yatoa vigezo vinavyotumika kuanzisha kituo cha Polisi

0
31

Waziri wa Mambo ya Ndani Nchi, Hamad Masauni amebainisha vigezo ambavyo hutumiwa na Serikali kuanzisha vituo vya Polisi katika maeneo yenye idadi kubwa ya watu  na maeneo yenye vitendo vya  uhalifu.

Akitoa majibu hayo kwa niaba ya waziri, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Jumanne Sagini ametaja vigezo hivyo bungeni Dodoma wakati akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Donge, Mohamed Soud.

“Vigezo vinavyotumiwa na Serikali kuanzisha vituo vya polisi, ni ongezeko la watu, ongezeko la matukio ya uhalifu, umbali kati ya kituo kimoja cha polisi na kingine na uwepo wa miundombinu ya Serikali,” amesema.

Vigezo vingine ni shughuli za kibiashara pamoja na maeneo ya kimkakati kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi, uwezo wa kibajeti na utayari wa wananchi na mamlaka zao za Serikali za Mitaa.

Aidha, ameongeza kuwa, nia ya uanzishwaji wa kituo cha Polisi huwasilishwa kwenye Kamati ya Usalama ya Wilaya, kisha mkoa, na shauri hilo huwasilishwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi kwa ajili ya utekelezaji ikiwa ni pamoja na mipango ya ujenzi, kupeleka askari na vitendea kazi.