Spika Tulia ahoji umuhimu wa Polisi kutangaza matukio ya mauaji ya raia

0
19

Spika wa Bunge, Dkt. Tulia Ackson ameishauri Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi kudhibiti taarifa za matukio ya mauaji zinazotolewa kwani kutangaza matukio hayo yanaweza kuwa kichocheo cha matukio mengine.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma Dkt. Tulia ameshauri kuwa ni vyema Wizara ikawataarifu Polisi walitazame jambo hilo kwa kina ikiwa kama kuna haja ya kuwatangazia wananchi pindi matukio hayo yanapotokea.

“Sisi tunajua mnafanya mambo mengi ili nchi yetu iwe salama na hamtuambii, sasa kwenye hili tujue kama ni muhimu kuambiwa na kama sio muhimu basi tuacheni wawe wanajua wale wanaohusika kwenye hilo eneo lao,” amesema.

IGP Wambura afanya mabadiliko ya Makamanda wa Polisi

Aidha, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Bunge, Sera na Uratibu, George Simbachawene amesema utafiti uliofanyika juu ya ongezeko la matukio ya mauaji nchini umeonesha sababu ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa matukio hayo ni pamoja na wivu wa mapenzi, imani za kishirikina, migogoro ya kugombea mali na ile ya ardhi.

Simbachawene amesema ipo haja ya kuwashirikisha wadau wote, na Serikali ipo haja ya kulingalia suala hilo kwa uzito na kutafiti kwanini matukio ya wananchi kujichukulia hatua mikononi yameendelea kuongezeka.