Tanzania yaiomba jumuiya ya kimataifa iisamehe madeni yake

0
14

Tanzania imeendelea kuziomba taasisi za fedha za kimataifa pamoja na nchi za Jumuiya ya Madola kufikiria kufuta kabisa madeni yaliyokopeshwa kwa nchi zinazoendelea ili fedha hizo ziweze kutumika kupambana na athari zilizotokana na Covid 19.

Ombi hilo limetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamamba Kabudi alipokuwa akimuwakilisha Rais Dkt. Magufuli katika mkutano wa Marais, Mawaziri Wakuu pamoja na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi na Serikali za Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa njia ya mtandao (video conference).

Tanzania imeyaomba mashirika ya fedha ya kimataifa pamoja na nchi za Jumuiya ya Madola zilizoikopesha (Tanzania) mbali na kutoa msamaha wa madeni waweze kufikiria kufuta kabisa madeni hayo ili kuziwezesha nchi zinazoendelea kuwa na fedha za kuboresha mifumo ya afya, pamoja na kupambana na athari zilizotokana na janga la Covid 19.

Ameongeza kuwa, nchi nyingi mara baada ya janga la covid 19 zilizuia utoaji wa dawa na vifaa tiba kwenda nje ya nchi kwa sababu dawa hizo walizihitaji kwa ajili ya matumizi yao wenyewe ndani ya nchi, na ndiyo maana nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi Kusini mwa Afrika (Sadc) tumeiomba India kwa upendeleo kutupatia dawa na vifaa tiba vya kukabiliana na janga la Corona.

Aidha, mkutano umejadili pia umuhimu wa teknolojia katika kupambana na Covid 19 na kuboresha mifumo ya afya na kwamba wakati umefika sasa teknolojia hiyo mahali popote ilipo ndani ya Jumiya ya Madola iweze kutolewa kwa nchi zote kwa gharama nafuu ili kuziwezesha nchi mbalimbali kutumia mifumo mipya ya kiteknolojia katika mifumo yake ya afya na kuziwezesha pia kupambana na Covid 19.

Send this to a friend