Tarime: Wanakijiji wafunga ofisi ya mtendaji kwa kutounga mkono kilimo cha bangi

0
18

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), imesema baadhi ya wakazi wa eneo la bonde la mto Mara wamelifanya eneo hilo kama eneo maalum kwa ajili ya kilimo cha bangi na hata wamediriki kufunga ofisi ya Kijiji wakimtuhumu mtendaji wa kijiji cha Nkerege kutounga mkono kilimo cha bangi.

Amesema hayo Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo baada ya kuteketeza hekari 807 za mashamba ya bangi wilayani Tarime mkoani Mara kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, Jeshi la Kujenga Taifa na askari mgambo.

Chuo chawekwa chini ya uangalizi kwa kutoa programu iliyofutwa

“Wamejimilikisha, hawaruhusu mtu yeyote asiye mkazi kuingia kwenye bonde kama sehemu ya kuficha uhalifu wao,” amesema Lyimo na kuongeza “wametishia kumdhuru yeyote atakayeingia ndani ya bonde hilo bila ridhaa yao. Pia, wamediriki kufunga ofisi ya kijiji wakimtuhumu mtendaji wa kijiji cha Nkerege kutounga mkono kilimo cha bangi.”

Aidha, amesema katika operesheni hiyo, watuhumiwa 11 wamekamatwa wakihusishwa na dawa hizo.

Chanzo: Habari Leo

Send this to a friend