Usajili wa Morrison ndani ya Simba SC waingia doa

0
26

Saa chache baada ya Klabu ya Simba kumtambulisha aliyekuwa mchezaji wa Yanga, Bernard Morrison kuwa ni mchezaji wao baada ya kukamilisha usajili, Yanga imeibuka na kusema kuwa nyota huyo ni mchezaji wao halali.

Katika taarifa yake, Uongozi wa Yanga umesema kuwa umeona kinachoendelea mitandaoni na kwamba inafuatilia jambo hilo kwa ukaribu na hatua kali na za mfano zitachukuliwa kwa pande zote zinazohusika.

“Mchezaji Bernard Morrison ana mkataba na Klabu ya Yanga hadi 2022 na shauri baina yake na klabu bado lipo mikononi mwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

Simba kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii imemtambulisha Morrison lakini haikueleza nyota huyo amesaini mkataba wa miaka mingapi.

Yanga ilimsajili Morrison mapema Januari mwaka huu akitokea klabu ya DC Motema Pembe ya nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.