Utafiti: Asilimia 63 ya Watanzania wanafurahia Serikali inavyosimamia uchumi

0
15

Ripoti ya Afrobarometer iliyotolewa na Taasisi ya Utafiti wa Sera kwa Maendeleo (REPOA), imeonesha kuwa takribani asilimia 63 ya idadi ya watu Tanzania wanafurahishwa na jinsi serikali inavyosimamia uchumi kwa ujumla.

Ripoti hiyo pia inaonyesha wananchi wanakabiliana na athari ya kuongezeka kwa bei ya bidhaa muhimu kama mafuta ya petroli, mbolea, unga wa ngano, na mafuta ya kupikia uliosababishwa na vikwazo vilivyowekwa kwa Urusi na nchi za Magharibi kutokana na mzozo unaoendelea nchini Ukraine.

Hali hiyo imekuwa ngumu zaidi kutokana na Marekani kutekeleza sera za fedha zilizolenga kudhibiti mfumuko wa bei, ambazo zina athari kwa thamani ya Dola ya Marekani duniani kote.

Licha ya changamoto hizi, matokeo ya Afrobarometer yanaonesha kuwa Watanzania wanaendelea kuwa na matumaini kuhusu mwelekeo wa uchumi wa nchi yao.

Ufahamu wa Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu mageuzi ya kiuchumi yanayolenga kuwavutia wawekezaji, umewapa Watanzania matumaini kwamba serikali ina dhamira ya dhati katika jitihada zake za kuchochea ukuaji wa kiuchumi na kuunda ajira.

Utafiti huo uliofanyika kati ya 2021-2023, ulilenga zaidi maeneo matano ikiwa ni pamoja na uchumi, utawala wa sheria, mfumo unaopendelewa wa utawala, demokrasia na imani katika taasisi za umma.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutolewa kwa matokeo ya utafiti, Mkurugenzi Mtendaji wa Repoa, Dkt. Donald Mmari amesema asilimia 82 ya walioulizwa wanakubaliana na utendaji wa serikali katika kukidhi mahitaji ya elimu huku asilimia 69 ya wananchi wakikubaliana na utoaji wa huduma za afya msingi na serikali.

Amesema licha ya kupungua kidogo ukilinganisha na utafiti uliopita, asilimia 65 ya washiriki bado wanachukulia juhudi za serikali katika kupambana na ufisadi kuwa za kupongezwa.

Send this to a friend