Utafiti: Hatari inayowakabili walaji wa kuku wa kisasa Dar es Salaam

0
19

Utafiti uliofanywa katika masoko ya Shekilango na Manzese jijini Dar es Salaam na kuchapishwa kwenye jarida la MDPI la Basel nchini Uswisi umebaini kuwepo kwa kiasi kikubwa cha mabaki ya sulphonamide na tetesaklin, antibayotiki zinazotumiwa zaidi na wafugaji kwenye maini ya kuku wa kisasa.

Utafiti huo uliochapishwa Septemba 8, ulihusisha sampuli 84 za maini ya kuku wa kisasa, ukilenga kuangalia kiasi cha mabaki ya dawa hizo kama kinaendana na kinachopendekezwa na viwango vya kimataifa.

Matokeo ya utafiti huo yameonesha maini yote 84 yalikuwa na mabaki ya tetesaklini huku 18 sawa na asilimia 21.4 yakiwa na mabaki ya sulphonamide na mengine 18 yakiwa na mabaki ya vyote.

Wakati mabaki ya sulphonamide yalikuwa ndani ya kiwango kinachokubalika kiafya, maini 76 sawa na asilimia 90.5 yalikuwa na kiasi kikubwa kuzidi kile kinachoshauriwa kuliwa na binadamu kwa siku, huku maini 13 sawa na asilimia 13.1 yalizidi kiwango cha juu cha tetesaklini, yakiwa na mikrogramu 300 kwa kila kilo moja.

Ufafanuzi wa Polisi video ya askari aliyechukua fedha kwa raia wa kigeni

“Kuwapo kwa kiwango kikubwa cha antibayotiki kwenye maini ya kuku kunahatarisha maisha ya walaji na kunaweza kusababisha usugu katika kutibu magonjwa yanayopaswa kutibiwa na dawa hizo,” imeeleza ripoti.

Ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza, watafiti wameshauri kuhakikisha kunakuwa na muda wa kutosha kwa dawa hizo kutumika mwilini kabla ya kuliwa, kupigwa marufuku hamasa ya matumizi ya dawa za kukinga, kutibu na kunenepesha mifugo pamoja na hatua ya kusitisha chanjo.