Uzembe wa dereva wasababisha vifo vya watu wanne Chalinze

0
13

Watu wanne wamefariki papo hapo baada ya gari yao aina ya Toyota Prado (T 104 CBU) lililokuwa likitokea Dar es Salaam kuelekea Same, Kilimanjaro kugongana uso kwa uso na Scania (T881 DWU) eneo la Chalinze mkoani Pwani.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Pius Lutumo amesema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa Toyota Prado kuhama kutoka upande wa kushoto wa barabara kwenda upande wa kulia bila kuchukua tahadhari.

Miili ya marehemu kwa sasa imehifadhiwa katika Zahanati ya Lugoba kwa ajili ya uchunguzi pamoja na kukabidhiwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi.

Waliofariki ni Nechi Msuya anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 45-50, dereva wa Prado, Dayana Mageta mwenye umri kati ya miaka 40-45 mfanyabiashara, Norah Msuya anayekadiriwa kuwa na umri kati ya 40-45, mwalimu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Tawi la Dar es Salaam pamoja na abiria wa kike ambaye jina lake halikufahamika anayekadiriwa kuwa na miaka 30-35.

Aidha, Jeshi la Polisi limewatahadharisha madereva kuepuka kutumia vileo pindi wanapoendesha vyombo vya moto, kwani imekuwa chanzo cha kusababisha ajali nyingi za barabarani.

Send this to a friend