Vodacom Tanzania yamkaribisha Nwanko Kanu ‘Twende Butiama’

0
4

Taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation imemkaribisha nchini Tanzania, gwiji wa Soka Barani Afrika kutoka nchini Nigeria, Nwankwo Kanu, katika ziara ya mbio za Twende Butiama mwaka 2024.

Kupitia taasisi yake ya Kanu Heart Foundation, Kanu ameelezea kufurahishwa kwake kuungana na juhudi zinazofanywa na Twende Butiama kama sehemu ya kumuenzi Baba wa Taifa wa Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

“Ni fursa ya kipekee sana kuwa sehemu ya kuleta mabadiliko kwa jamii hasa katika eneo la afya ambalo linanigusa sana. Upekee huu umenifanya nije Tanzania kuwa mmoja wa washiriki katika ziara hii kwa sababu ni jambo jema,” amesema Kanu katika mkutano na wanahabari uliofanyika Makao Makuu ya Vodacom Tanzania jijini Dar es Salaam mnamo tarehe 13 Septemba, 2024.

Mbio za Twende Butiama zilianzishwa mwaka 2019 na kikundi cha waendesha baiskeli, ili kuadhimisha upendo wa Mwalimu Nyerere wa kuendesha baiskeli na maono yake kimaendeleo katika maeneo matatu muhimu ambayo ni elimu, afya, na utunzaji wa mazingira ambayo yanaweza kuwasaidia Watanzania kupiga hatua kijamii na kiuchumi.

Mkurugenzi wa Mahusiano na Vodacom Tanzania Foundation, Zuweina Farah amesema, “Tumefurahi sana Nwankwo Kanu kujumuika nasi katika mbio zetu za Twende Butiama mwaka huu, kwa kushirikiana na taasisi yake ya Moyo tunaamini itatusaidia katika msafara wetu ambapo tunatoa huduma za afya kwa magonjwa yasioambukizwa  katika maeoneo kadha ya mikoa 12 tutakayopita.”

Naye mwanzilishi wa mbio za baiskeli za Twende Butiama, Gabriel Landa amesema mbio hizo zitaambatana na utoaji wa huduma kwa jamii zaidi ya afya kama vile kuchangia elimu, na kuhamasisha upandaji miti, na wanatoa nafasi kwa washiriki zaidi kujiandikisha ili kushiriki kampeni hiyo.

Send this to a friend