Waziri Gwajima aagiza madaktari wanaopotosha kuhusu Corona wawajibishwe

0
18

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima ameliagiza Baraza la Madaktari Tanzania (MAT) kuwachukulia hatua zikiwemo za kinidhamu madaktari wanaosambaza taarifa potofu kuhusu Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19) pamoja na chanjo zake.

Dkt. Gwajima ametoa agizo hilo jijini Mwanza kupitia hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel kwenye ufunguzi wa mkutano wa 53 wa kisayansi pamoja na mkutano mkuu wa mwaka wa MAT.

Amesema mtaalamu yeyote atakaayeshindwa kuthibitisha atakachosema kuhusu UVIKO19 na chanjo zake atachukuliwa hatua, mpango unaolenga kudhibiti taarifa potofu ambazo huwatia hofu wananchi na kupelekea kutochukua tahadhari ikiwemo kutotaka chanjo.

Kwa upande wake Rais MAT, Dkt. Shadrack Mwaibambe amesema taaarifa zimekuwa zikisambaa kuhusu ugonjwa huo na chanjo, lakini wataalamu wataendelea  kutoa taarifa sahihi, ili wananchi wafanye uamuzi sahihi. 

“Bado tuna nafasi sisi kama wanataaluma kueneza habari njema… Kuna kundi kubwa la Watanzania ambalo halijafanya maaamuzi [kuhusu chanjo ya UVIKO19]. Changamoto au madukuduku yam hayazidi matano ambayo ni nguvu za kiume, ujauzito, kunyonyesha, uzazi, zote zitapatiea majibu,” ameeleza.

Baadhi ya washiriki wa mkutano huo wamewasihi Watanzania kutokuwa na hofu kwani chanjo ni salama.