Waziri Kairuki: Waombaji wa ajira 419 walidanganya kuwa ni walemavu

0
13

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Angellah Kairuki amesema kati ya waombaji 171,916 walioomba ajira katika kada ya ualimu na afya kupitia wizara hiyo, waombaji 1,169 walijitambulisha kuwa ni walemavu ambapo zaidi ya watu 419 hawakuwa na ulemavu kama walivyodai.

Akizungumza leo kuhusu matokeo ya nafasi za ajira zilizotangazwa Aprili 12, 2023, amesema baada ya kufanya uchunguzi wamebaini kuwa kati ya waombaji 64 waliojitambulisha kuwa na ulemavu wa ngozi, ni waombaji 24 tu ndio walisema ukweli huku 40 wakidanganya.

Vigogo wa Shirika la Bima la Taifa wakabiliwa na mashitaka 365

Hata hivyo amesema kati ya waombaji waliojitokeza ni waombaji 18,449 tu ndio wamechaguliwa na kupangiwa vituo vya kazi baada ya kukidhi vigezo vya kitaaluma na taratibu za uombaji ambapo kada ya afya ni 5,319 na ualimu ni 13,130 na kati yao wenye mahitaji maalum ni 111 sawa na asilimia 0.84.

Aidha, katika kada ya afya, nafasi 8,070 ndio zilizotangazwa lakini zilizopatikana na kukidhi vigezo ni 5,319 na kufanya nafasi 2,751 kuendelea na mchakato wa kutafuta wengine.

Send this to a friend