Waziri Mkenda: GPA isiwe kigezo pekee cha ajira vyuo vikuu

0
14

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema badala ya kuangalia ubora wa ufaulu yaani ‘GPA’ katika ajira za vyuo vikuu, waajiriwe kwa kupimwa uwezo wao kwa kufanya usaili.

Ameyasema hayo leo Desemba 12, 2022 katika mahafali ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Jijini Dar es salam akisisitiza kuwa kuangalia ufaulu pekee wa wanafunzi haitoshi kuboresha elimu badala yake ni muhimu kuongeza vigezo hivyo katika mapitio ya sera na mabadiliko ya mitaala.

Amesema wakati Serikali inaongeza udahili wa wanafunzi haitakuwa tayari kuona ubora unapungua, hivyo Serikali inaendelea na mkakati wake wa kuhakikisha ubora wa elimu hususani katika vyuo vikuu unaimarika.

CCM: Vyama vya upinzani viwe huru kususia uchaguzi

“Zamani ilikuwa rahisi kuwa Profesa ukiandika tu kwenye magazeti unakuwa Profesa lakini kwa sasa vigezo vya kuwa Profesa vimezidi kuwa vigumu kwa sababu tunataka maprofesa wetu wawe sawa na wale wa nchi zingine,” amesema

Aidha, Waziri Mkenda ameongeza kuwa Serikali kwa sasa inaendelea na ujenzi wa kampasi mpya za vyuo vikuu katika Mikoa 14 ambayo haina vyuo vikuu ukiacha vyuo huria. Mikoa hiyo ni pamoja na Tabora, Katavi, Kigoma, Kagera, Singida, Manyara, Lindi, Rukwa, Mwanza, Simiyu, Tanga, Ruvuma, Shinyanga na Dodoma.

Send this to a friend