Waziri Mkuu: Rais Samia anataka kuona biashara zinafanywa kwa uhuru

0
17

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema lengo la Rais Samia Suluhu Hassan ni kuona kila mfanyabiashara nchini anafanya shughuli zake kwa uhuru na amani katika nchi yake bila kuwepo kwa vikwazo vyovyote.

Ameyasema hayo wakati akizungumza na wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo baada ya kutangaza mgomo ulioanza mapema leo wakilalamikia kamata kamata ya mizigo inayofanywa na Mamlaka ya Mapato (TRA), kupinga sheria ya usajili wa stoo na urasimu unaodaiwa kufanywa bandarini.

Waziri Mkuu aagiza TRA kusitisha kikosi kazi cha kukusanya kodi Kariakoo

“Mheshimiwa Rais [Samia Suluhu] anataka kuona Mtanzania aliyeamua kufanya shughuli yoyote ile, biashara, kilimo, kuwekeza kwenye viwanda na maeneo mengine afanye kwa uhuru mkubwa akiwa ndani ya nchi yake,” amesema Waziri Mkuu.

Aidha, Waziri Mkuu ameitisha kikao kwa lengo la kujadili matatizo ya wafanyabiashara ambao watawakilishwa na wawakilishi wao pamoja na Serikali ikiongozwa na Waziri Mkuu, mawaziri pamoja na viongozi wa TRA ili kupata ufafanuzi wa juu ya sakata hilo.

Hata hivyo amewaonya viongozi kutoka TRA kuacha kuonea wafanyabiashara ili waweze kustawi katika biashara zao na nchi iweze kupata mapato yake ili kujenga kwa pamoja uchumi wa taifa.

Send this to a friend