Zanzibar: Ombaomba wapewa eneo la kufanyia biashara

0
14

Mkuu wa Wilaya Mjini, Rashid Msaraka kwa kushirikiana na watendaji kutoka kitengo cha ustawi wa jamii amesema watahakikisha wanafanya operesheni za mara kwa mara kuwasaka ombaomba wote walioko katika mji huo.

Ameyasema hayo baada ya kitengo cha ustawi wa jamii kuwakamata watu 19 wanaojihusisha na kazi ya kuomba, ambao tisa wamerejeshwa Tanzania Bara, wawili wamechukuliwa na jamaa zao na sita wamepatiwa eneo la kufanya biashara katika Soko la Kibandamaiti, huku wawili wakihifadhiwa nyumba salama.

Aidha, amesema katika uchunguzi uliofanywa wamebaini kuwa, ombaomba wengi wametoka nje ya Zanzibar na kuongeza kuwa, haipendezi kuwaona katika kila pembe ya mji huo na watahakikisha wanaweka mji safi ukiwa hauna ombaomba.

Miongoni mwa walionaswa katika operesheni hiyo Amina Fredrick aliyesema ameamua kufanya kazi hiyo kwa lengo la kujipatia fedha ambazo anazituma kijijini kwao kwa ajili ya kuimarisha mtaji wa biashara yake ya duka.

Hata hivyo amewataka watu wenye ulemavu wanaotoka nje ya Zanzibar na ambao wanatumia vibaya ulemavu wao kujipatia kipato kuwa, wanapoingia visiwani hapo wafuate taratibu zilizowekwa na serikali.

 

Send this to a friend