ZFF yapiga marufuku kampuni za ‘betting’ kuingiza Ligi Kuu ya Zanzibar

0
23

Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF) limezitaka kampuni za kamari nchini kuondoa mara moja Ligi Kuu ya Zanzibar (PBZ Premier League) katika orodha ya betting kwenye kampuni zao za kamari kwani ni makosa kwa mujibu wa sheria.

Katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari imesema kuwa Zanzibar haijatoa ruhusa ya kampuni za kamari na pombe kuwa ni sehemu ya udhamini na kushiriki katika michezo Visiwani humo.

“Kitendo cha baadhi ya kampuni za kamari kuiweka ligi ya Zanzibar kwenye huduma zao watambue kuwa ni makosa makubwa kwa mujibu wa miongozo ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,” imesema.

Aidha, imesema ZFF inafuatilia kwa ukaribu jambo hilo na kuchukua hatua stahiki kwa kuanza kushirikiana kwa ukaribu na vyombo husika ili kupatikana kwa mustakabali sahihi kwa maslahi mapana ya mpira wa miguu visiwani humo.