in , ,

Uwanja wa KIA warudishwa serikalini baada ya miaka 25

Serikali imetangaza leo kuwa hatimaye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) utakabidhiwa kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) inayomilikiwa na Serikali kuanzia kesho, Novemba 10 2023.

Hata hivyo, taarifa kuhusu wamiliki wa awali wa Kampuni ya Uendelezaji na Uendeshaji wa Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro (KADCO), kampuni iliyosimamia uwanja huo kwa miaka 25 na kukusanya mapato ya mamilioni ya dola bila kulipa ada ya mkataba, bado haijawekwa wazi.

Uwanja wa Ndege wa KIA ni wa tatu kwa shughuli za usafirishaji nchini Tanzania, na pia ni lango kuu kuelekea katika vivutio vya utalii hususani mbuga za wanyama.

Mnamo Machi 11, 1998, Kampuni ya KADCO ilisajiliwa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), ikiwa na wamiliki wasiojulikana sana ambao ni kampuni za Mott MacDonald International Ltd (asilimia 99) na Inter Consult Ltd (asilimia 1).

Miezi mitatu baada ya usajili wa KADCO, Julai 17, 1998 kampuni hiyo iliingia katika makubaliano mapya ya umiliki, ambapo serikali ya Tanzania ilipata asilimia 24 ya hisa za kampuni hiyo, Mott MacDonald International Ltd (asilimia 41.4), South Africa Infrastructure Fund (asilimia 30) na Inter Consult (T) Ltd (asilimia 4.6).

Novemba 10,1998, miezi 8 tu baada ya kuanzishwa kwa KADCO, kampuni hiyo ilisaini mkataba wa miaka 25 na serikali ya Tanzania, ikimpa haki ya kuendeleza na kusimamia uwanja wa KIA, licha ya kutokuwa na rekodi au uzoefu wa awali wa uendeshaji wa uwanja wa ndege.

Uganda kupitisha mafuta Bandari ya Dar es Salaam baada ya kushindwana na Kenya

Mwaka 2006, serikali ilifanya tathmini ya utendaji wa KIA na kugundua mambo kadhaa ya kushangaza, ikiwa ni pamoja na kutofanyika kwa uwekezaji katika miundombinu ya KIA, makubaliano hayakuwa na kipengele cha ada ya mkataba na kutokuwepo kwa kipengele cha kusitisha mkataba katika makubaliano.

KADCO haikulipa ada yoyote ya mkataba kwa serikali kwa kusimamia uwanja wa ndege licha ya kukusanya mapato. Makubaliano yalikuwa na kipengele cha kuendeleza mkataba baada ya miaka 15 mara baada ya kumalizika kwa miaka 25 ya mkataba.

Makubaliano pia yalizuia ujenzi wa uwanja wa ndege wa kimataifa ndani ya umbali wa kilomita 240 kutoka upande wowote wa KIA, na hivyo kumpa KADCO haki pekee ya kusimamia uwanja wa ndege wa kimataifa katika eneo hilo.

Wakati serikali ilipotaka marekebisho ya vifungu vya mkataba, wamiliki wa KADCO walikataa marekebisho hayo, na mwaka 2009 serikali iliamua kununua hisa za wamiliki wa kampuni na kupata umiliki wa asilimia 100 wa KADCO. Bado haijulikani kiasi gani serikali ililipa kwa wamiliki wa kampuni ili kuachia umiliki huo.

Licha ya serikali kuchukua umiliki wa asilimia 100 wa KADCO, kampuni hiyo iliendelea kusimamia KIA licha ya maswali kutoka kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Bunge kuhusu hatma ya mapato yaliyokusanywa na KADCO kama msimamizi wa uwanja wa ndege.

Rais Samia afanya uteuzi wa viongozi na kuvunja Bodi ya TCRA

Miaka 8 jela kwa kumuua mchepuko wa mumewe