in ,

Mawasiliano ya Barabara ya Lindi – Dar kurejea Mei 9

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amewatoa hofu wananchi, wasafiri na wasafirishaji kuwa kufikia Mei 9, mwaka huu kazi ya kurudisha mawasiliano ya barabara ya Lindi – Dar es Salaam itakuwa imekamilika.

Ameeleza hayo Nangurukuru wilayani Kilwa ambapo ameweka kambi kuhakikisha anasimamia timu ya watalaamu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na makandarasi, kuhakikisha barabara hiyo iliyoharibiwa na mvua kubwa zilizonyesha zikiambatana na kimbunga Hidaya inatengemaa ndani ya saa 72.

“Niendelee kuwatoa hofu wananchi na wasafiri wanaotumia barabara hii inayounganisha mikoa ya Kusini, tangu jana nimepiga kambi huku, nilianzia Somanga na sasa hivi tupo upande huu wa Nangurukuru, kama mnavyoona pande zote wanaendelea na kazi, bado tunaamini ndani ya saa 72, kufikia Alhamisi tutakuwa tumekamilisha kazi ya kurudisha mawasiliano ya barabara hii,” amesema Bashungwa.

Aidha, amemuagiza Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Eng. Mohamed Besta kuhakikisha anaongeza idadi ya malori yanayosomba mawe pamoja na mitambo inayotumika kupakia mawe katika magari ili kuongeza kasi ya kujaza vifusi katika eneo la barabara yaliyosombwa na maji.

BASATA yatangaza kuwataja wasanii ambao hawana vibali baada ya siku saba

Mtu mmoja afariki Polisi wakidhibiti wavamizi mgodi wa North Mara